ULEMAVU SI MKOSI WALA LAANA.
| 
WANAUME
  WATELEKEZA WATOTO WALEMAVU ARUMERU  | 
| 
Wanawake
  wasukumiwa mzigo  
Tatizo la wanaume kuwatelekeza
  watoto wao wenye ulemavu, limetajwa kukithiri katika Kijiji cha Ambureni,
  Wilaya ya Arumeru, mkoani Arusha. 
Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa
  na JAMHURI
  hivi karibuni, umebaini kuwapo kwa
  familia zaidi ya 15 zenye watoto walemavu zilizotelekezwa na waume, hivyo
  wanawake kuachiwa mzigo wa kuzilea. | 
| 
Tabia hiyo imesababisha familia
  hizo kuishi katika mazingira magumu ikiwa ni pamoja na kuishi katika nyumba
  za kupanga, huku zikiwa hazina kazi za kujipatia kipato.  Mateso
  yanayowakabili wanawake hao yanatokana na kujifungua watoto wenye ulemavu,
  kwani bila kujifungua watoto hao wangeendelea kuishi na waume zao. 
Zeana Athuman, mkazi wa Ambureni
  ambaye pia ni mwanawake aliyeathirika na hali hiyo, anasema mume wake
  aliondoka nyumbani baada ya kujifungua mtoto mwenye ulemavu. 
“Baada ya kujifungua mume wangu
  alitoroka nyumbani na akaniacha nikiwa peke yangu katika hali ngumu
  kimaisha,” anasema Zeana. 
Alijifungua mtoto mwenye ulemavu
  wa kutoona, kutotembea, kutosikia na kutozungumza. 
“Mume wangu alimwona mwanangu kama
  mkosi ndani ya familia, alinikimbia mtoto akiwa na mwezi mmoja,” anasema. 
Anaongeza kwamba tangu mumewe
  amkimbie ni miaka 11 imepita sasa, jambo linaloendelea kufanya maisha yake na
  mtoto wake kuwa magumu zaidi. 
Zeana anasema ili kukidhi mahitaji
  yake na mtoto wake kwa siku, analazimika kumuacha mwanaye huyo kwa majirani
  aweze kutafuta fedha za kujikimu. Changamoto iliyopo ni kwamba muda mwingi
  mtoto huyo hufungiwa ndani wakati wote ambao mama yake hutoka kwenda kutafuta
  riziki. 
JAMHURI pia inakutana na mtoto anayetajwa kwa jina moja la
  Terezia (6) mwenye ulemavu anayeishi na bibi yake. Taarifa zinasema baba
  mzazi wa mtoto huyu aliondoka nyumbani hapo baada ya kuona mtoto wake ni
  mlemavu. 
Wakati baba akiwa amemtoroka
  mwanaye, mtoto huyu anatajwa kuwa katika mazingira magumu zaidi kwani hata
  mama yake naye hulazimika kuondoka nyumbani na kumuacha akiwa peke yake. 
“Mtoto huyu alizaliwa akiwa mzima,
  baada ya miezi saba hali yake ilianza kubadilika akawa haoni wala kusikia
  ndipo baba mzazi alipoamua kuondoka nyumbani. 
“Mama mzazi naye alianza kumficha
  ndani kwa madai kuwa anaogopa watu kumsema amezaa mtoto mlemavu. 
“Baada ya majirani kugundua tatizo
  hilo waliamua kwenda kumtoa ndani kwa nguvu na kuanza kumshindisha nje kama
  watu wengine,” anasema bibi wa Terezia bila kutaja jina lake. 
Kutokana na changamoto
  zinazowakabili wanawake wenye watoto walemavu kijijini hapo, hatimaye
  wamebuni mbinu za kulea watoto wa watu (yaya) ili wapate kipato cha kuendesha
  maisha yao. 
Mwalimu wa kituo cha kulelea
  watoto wenye ulamavu katika Shule ya Msingi Moivaro wilayani Arumeru, Leah
  Ndaga, anataja changamoto zinazowakabili katika kazi hiyo.  Mwalimu Leah
  anasema kwamba kwa muda mrefu sasa wananchi wamekuwa wakibeza aina ya kazi
  wanayoifanya kwa madai kuwa wanapoteza muda kukaa na watoto wenye ulemavu. 
“Tunatoa elimu kwa jamii na maeneo
  yanayotuzunguka kuwa watoto hawa ni sehemu ya jamii yetu. Tunaiomba jamii
  iwachukulie kama sehemu yao isiwatenge badala yake iwasaidie wanapohitaji
  msaada ukiwamo wa kwenda shuleni,” anasema. 
Wakati wakiendelea na juhudi za
  kusaidia miundombinu ya kwenda eneo moja hadi jingine, kituo hicho kina
  watoto 47. Kati ya hao, watoto watatu wana ulemavu wa macho huku wengine
  wakiwa na ulemavu wa kutosikia, kutoongea na kutotembea. 
Mwenyekiti wa Kitongoji cha
  Msovero, Sioni Mathayo, akizungumzia changamoto hiyo anasema imekuwa vigumu
  kuwasaidia watoto hao kutokana na kutokuwa na kipato cha kutosheleza
  mahitaji. 
“Serikali ya kitongoji hatuna
  mafungu ya kusaidia watoto walemavu. Tunaomba viongozi wajaribu kuangalia
  upya jinsi ya kuziwezesha serikali za vitongoji ambazo zipo na wananchi,’’
  anasema Mathayo. 
Pamoja na kutokuwa na bajeti,
  Mwenyekiti huyo anabainisha kuwa kama kiongozi alichukua jukumu la kupeleka
  matatizo hayo kwenye uongozi wa juu ili kupata msaada wa namna ya kuwabana
  wanaume hao wasizikimbie familia zao. 
Anasema juhudi nyingine
  zinazofanywa ni za kuwapatia msaada kupitia Kituo cha Aston Vision kilichopo
  kijijini hapo, ambacho hutoa elimu kwa watoto yatima na wanaoishi katika mazingira
  magumu. 
Mwasisi wa kituo hicho, Aston
  Simoni, anasema lengo la kuanzisha kituo hicho lilitokana na kijiji hicho
  kuwa na watoto wengi wenye ulemavu na wanaoishi katika mazingira hatarishi. 
“Hapa tunapata msaada kutoka kwa
  wadau wa nje na ndani ya nchi ambao hutusaidia chakula, magodoro na dawa za
  kuongeza vitamini kwa watoto yatima na wale wenye walemavu. | 
Comments
Post a Comment