| 
WADAU
    mbalimbali wa elimu yakiwemo mashirika binafsi na ya kiserikali, wamekuwa
    wakitupia lawama kwa wazazi na walezi wa watoto wenye ulemavu kwa kushindwa
    kuwapeleka shuleni. 
Wamekuwa
    wakitoa madai hayo bila ya kuzifanyia kazi changamoto zinazowakwamisha
    wazazi hao kuwapa watoto hao haki yao ya msingi ya kupata elimu. 
Wengi
    wa watoto wenye ulemavu toka vijijini wamekuwa wakiishi mazingira magumu
    kutokana na hali duni za wazazi wao. 
Wazazi
    nao wamekuwa wakisubiri hadi watoto wao walemavu watambuliwe na mashirika
    au wafadhili ndipo wasaidiwe kupata elimu. 
Jambo
    la kutegemea msaada si rahisi kwa kila mzazi, kwani hata wafadhili hawana
    fedha za kutosha kuhudumia walemavu wote wa Tanzania. 
Hivyo,
    kuwategemea wafadhili kutasababisha watoto wengi, hasa vijijini kuendelea
    kuishi bila kupelekwa shuleni. 
Mwalimu
    Mkuu wa Shule ya Msingi Kongowe, Wilaya ya Kibaha mkoani Pwani, Beatus
    Lingumbuka anasema shule yake ina wanafunzi 1,502; wavulana 789 na
    wasichana 713. 
Anasema
    katika kitengo cha elimu maalumu kuna wanafunzi 42 wa mtindio wa akili,
    viziwi, albino na walemavu wa viungo wawili. 
Akielezea
    juu ya wanafunzi ambao wana ulemavu, mwalimu huyo anasema baadhi yao
    wamekuwa wakikatisha masomo mara kwa mara kutokana na kukosekana kwa watu
    kutoka katika familia zao kuwahudumia. 
Kila
    mtoto anahitaji mtu wa kumpeleka shule asubuhi na kumchukua ili kurudi
    nyumbani mara baada ya muda wa masomo kila siku. 
Suala
    hili linaweza likaoneka kama ni jambo rahisi kwa watu wa mijini, lakini ni
    gumu sana kwa mkulima au mfugaji wa kijijini. 
Mwalimu
    huyo anaendelea kueleza kuwa changamoto kubwa wanayokabiliana nayo
    wanafunzi wenye ulemavu ni kushindwa kujitegemea kwa kutembea wenyewe hadi
    shuleni. 
Watoto
    hao wanahitaji kusindikizwa na anapokosekana msindikizaji ndipo wanapofikia
    hatua ya kukatisha masomo. 
“Katika
    shule yangu kitengo cha elimu maalum, kilianza miaka kumi iliyopita lakini
    kikubwa kinachosababisha wanafunzi wenye ulemavu kushindwa kuendelea na
    masomo yao ni kukosa wasindikizaji,” anasema Lingumbuka. 
Pia
    ukosefu wa chakula shuleni kwa watoto walemavu limekuwa tatizo kubwa kwani
    wakiona hakuna uji wala chakula hawaendelei kuja shule, wanagoma na
    kuendelea kubaki nyumbani,” anasema. 
Walimu
    wanaofundisha wanafunzi wenye ulemavu wa mtindio wa akili na kutosikia
    (Viziwi), Damaris Mkonye na Getrude Kavishe wanasema mbali ya changamoto
    hizo, huduma muhimu kwa wanafunzi hao ni tatizo. 
Wanasema
    vifaa vya michezo na ziara za kimasomo vinasababisha wanafunzi hao
    kushindwa kuendelea na masomo. 
Mwalimu
    Kavishe ambaye anafundisha walemavu wenye mtindio wa akili, anasema katika
    darasa lake anakabiliwa na ukosefu wa vifaa vya kufundishia pamoja na vya
    michezo. 
“Unajua
    ili hawa watoto wenye ulemavu waendelee kuja shuleni, ni lazima kuwepo na
    vivutio kama vifaa vya kutosha kwa ajili ya michezo. 
“Pia,
    chakula kiwepo na wapate muda wa kucheza. Kama hakuna vitu hivyo, huwaoni
    umuhimu wa kuwa shuleni,” Getrude anasema. 
Serikali
    pia haijatenga fungu la kutosha kuwawezesha walimu kuzunguka nyumbani kwa
    watoto hao kuwafuatilia juu ya masomo wanayofundishwa. 
“Unajua
    katika darasa la walemavu ratiba yao inaelekeza siku nne ni za kuja shuleni
    kufundishwa lakini siku moja ambayo ni ya tano katika juma tunatakiwa
    walimu tuwatembelee nyumbani kwao, ili tujue kama tunayowafundisha
    wanafanya kama inavyotakiwa. Sasa fedha za kutuwezesha kuwafikia hakuna,”
    anafafanua. 
Kwa
    upande wake mwalimu wa wanafunzi viziwi, Mkonye anaelezea juu ya uelewa
    mdogo wa wazazi wa watoto wenye ulemavu. 
Anasema
    wazazi wengi wanawanyima haki yao ya msingi kwa kutowapeleka shuleni kupata
    elimu sawa na wengine. 
Mkonye
    anasema baadhi ya wazazi wa watoto wenye ulemavu wamekuwa na tabia ya
    kuwaficha watoto wao. Jambo linalosababisha waendelee kuishi bila ya
    kuwasomesha wakidhani watoto walemavu hawawezi kumudu masomo sawa na wale
    ambao hawana ulemavu. 
Anawataja
    baadhi ya wanafunzi ambao wameacha masomo kutokana na sababu mbalimbali
    akiwemo mwanafuzi wa kike aliyekatisha shule mwaka 2010 mkazi wa Miembe
    Saba. 
Anasema
    wazazi wake hawakuona umuhimu wa kuendelea kumsindikiza shuleni. 
Mwalimu
    huyo anasema wazazi wa binti huyo kiziwi walimkatisha masomo akiwa darasa
    la tano. Baadae walimpeleka kufanya kazi za ndani jambo waliloona ni muhimu
    kuliko kusoma. 
Wengine
    waliokatisha masomo ni pamoja na msichana aliyeacha shule akiwa darasa la
    tatu mwaka 2009 kutokana na kukosa mtu wa kuendelea kumsindikiza shuleni. 
“Mvulana
    mmoja, mkazi wa Mwambisi nae alikatishwa masomo akiwa darasa la pili mwaka
    2009 kwa kukosa msindikizaji wa kumfikisha shuleni,” anasema. 
Aidha,
    anasema kuwa mwanafunzi mmoja mkazi wa Visiga nae alishindwa kuanza masomo
    kutokana na umbali mrefu kutoka nyumbani kwao na kukosekana kwa mtu wa
    kumsindikiza. 
Mwalimu
    Mkuu wa shule hiyo, ameomba serikali iongeze bajeti hasa kwenye vituo vya
    walemavu ili viweze kununua vifaa na kupika chakula kitakachosaidia
    kuwavutia walemavu kuendelea na masomo. 
Serikali
    ikiongeza bajeti itawasaidia kwa kuwa wazazi kwa sasa hawachangii kabisa
    swala la chakula kwa watoto wao. Hivyo, fedha za ruzuku kwa ajili ya
    maendeleo ya shule zinapoisha hawana sehemu nyingine ya kupata fedha za
    kununulia chakula kwa wanafunzi hao. 
Hivi
    sasa shule hiyo inapika uji kwa ajili ya watoto wenye ulemavu ili kuendelea
    kuwavutia kuipenda shule na kuendelea kuhudhuria katika vipindi vya masomo. 
Changamoto
    nyingine ni ya uhaba wa vyumba vya madarasa kwa watoto wenye ulemavu. Kwa
    sasa wanatumia chumba kimoja kwa madarasa matatu badala ya kila darasa kuwa
    na chumba chake. 
Mwalimu
    huyo mkuu anawasihi pia wazazi kutambua umuhimu wa elimu kwa watoto wenye
    ulemavu na kuondokana na dhana potofu ya kudhani kila mtoto anayezaliwa
    akiwa mlemavu amerogwa. 
Hata
    hivyo, imebainika kuwa baadhi ya wazazi wa watoto wenye ulemavu wamekuwa wakificha
    taarifa za watoto wao. 
Wazazi
    hao wamedai kuwa wamekuwa wakitembelewa mara nyingi na baadhi ya asasi,
    lakini hawarudi kuwapatia misaada na hivyo kuwakatisha tamaa. 
Katibu
    wa watu wenye ulemavu katika Wilaya ya Kisarawe, Pwani, Ibrahim Tully
    anasema katika maeneo ya vijijini bado kuna muamko mdogo wa wazazi
    kuwapeleka shule walemavu. 
Anasema
    wazazi wanadai kuwa watoto walemavu hawawezi kufanya chochote. 
Tully
    anasema ipo haja ya serikali kulichukulia umuhimu wa kipekee swala hilo ili
    kuwezesha kila mtoto mwenye ulemavu kupata haki yake ya elimu. 
Anasema
    serikali iachane na mtindo wa kuzitegemea asasi pekee kuwaibua watoto hao
    na kuwasaidia. 
Mbunge
    wa Kisarawe, Seleman Jafo, mdau wa elimu, aliyetembelea Kijiji cha Chole
    kusaidia walemavu amezisihi asasi za kiraia kuendelea kutoa misaada ya
    baiskeli na vifaa vingine. 
Anasema
    vifaa hivyo vitawawezesha watoto wenye ulemavu kufika shule. 
Jafo
    pia anaeleza kuwa baadhi ya watoto wenye ulemavu waishio vijijini
    wanashindwa kupata haki stahiki kutokana na wazazi wao kuwaficha. 
Anadai
    kuwa kuna mila na desturi, mkoani Pwani ya kudhani mtoto mwenye ulemavu
    anasababisha mikosi kwenye familia. | 
Comments
Post a Comment